UVCCM
Tafadhali subiri...
UMOJA WA VIJANA WA CCM (UVCCM)

ABUYA AWEKA MSISITIZO KWA VIJANA WA CCM KUKITETEA CHAMA NA VIONGOZI WAKE

31 Jan, 2026 40 Machapisho
Mwenyekiti wa Umoja wa Vijana wa Chama Cha Mapinduzi (UVCCM) Mkoa wa Kigoma, Ndugu Emanuel Abuya, amewataka vijana wa CCM kuendelea kuwa mstari wa mbele katika kutetea, kulinda na kudumisha misingi, sera na uongozi wa Chama Cha Mapinduzi, akisisitiza kuwa hilo ni jukumu la msingi na la kihistoria kwa jumuiya ya vijana.
Ndugu Abuya ametoa kauli hiyo leo katika Kata ya Bangwe, Wilaya ya Kigoma Mjini, wakati wa maadhimisho ya miaka 49 ya kuzaliwa kwa Chama Cha Mapinduzi (CCM), yaliyoandaliwa na Umoja wa Vijana wa CCM Wilaya ya Kigoma Mjini, yakihusisha viongozi, wanachama na vijana wa CCM.
Akizungumza kama mgeni rasmi katika maadhimisho hayo, Mwenyekiti  wa UVCCM Mkoa wa Kigoma alieleza kuwa vijana wana nafasi kubwa na ya kipekee katika kukilinda chama dhidi ya upotoshaji, propaganda na hoja zinazolenga kupotosha umma, hasa katika mazingira ya ushindani wa kisiasa na matumizi makubwa ya mitandao ya kijamii.
Alisisitiza kuwa, pamoja na kushiriki shughuli za maendeleo na ujenzi wa chama, UVCCM ina wajibu wa msingi wa kuwalinda na kuwatetea viongozi wake katika ngazi zote, akiwataja hususani Mwenyekiti wa CCM na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, pamoja na wabunge na madiwani wa chama hicho.
“Ni wajibu wetu kama vijana wa CCM kuwa walinzi wa chama chetu, sera zake na viongozi wake. Tunapaswa kusimama imara kuutetea uongozi wetu na mwelekeo wa chama kwa maslahi mapana ya taifa letu,” alisema Ndugu Abuya.

Katika kuadhimisha tukio hilo, vijana wa CCM walishiriki pia zoezi la upandaji miti, ikiwa ni ishara ya kuenzi mazingira, kudumisha uhai kwa vizazi vya  sasa na baadaye, pamoja na kuonesha dhamira ya chama katika kulinda rasilimali za asili na kuchangia maendeleo endelevu ya taifa.
Upandaji wa miti  ni ishara ya ukuaji, uimara na uendelevu wa Chama Cha Mapinduzi, sambamba na kuimarisha uzalendo wa vijana katika kulinda siasa safi, mazingira na mustakabali wa Tanzania.
Maadhimisho ya miaka 49 ya CCM yanaendelea kuwa jukwaa muhimu la kuwakumbusha vijana wajibu wao wa kihistoria wa kuendeleza misingi ya chama, kuimarisha mshikamano na kuhakikisha CCM inaendelea kuwa chama imara, chenye dira na kinachoendelea kuwatumikia Watanzania kwa uadilifu na maendeleo.

#Kazi na Utu, Tunasonga Mbele