VIJANA VYUONI GOMBEENI UONGOZI UVCCM
Dodoma, 03 Januari 2026 – Katibu Msaidizi wa Idara ya Uhusiano wa Kimataifa, Vyuo na Vyuo Vikuu wa UVCCM, Ndugu Mabula Marco Mabula, amewahimiza vijana wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) wanaosoma katika vyuo na vyuo vikuu nchini kujitokeza kwa wingi kugombea nafasi mbalimbali za uongozi ndani ya Seneti za Vyuo na Vyuo Vikuu kupitia jumuiya ya UVCCM.
Akizungumza katika Ofisi za Makao Makuu ya UVCCM, Tambuka Reli jijini Dodoma, Mabula amesema fomu za kugombea zitatolewa kuanzia Jumatatu tarehe 05 hadi 07 Januari 2026 katika ofisi za Makatibu wa UVCCM wa mikoa yote ya Tanzania Bara na Zanzibar.
Nafasi Zinazogombewa
Mabula ameeleza kuwa nafasi zitakazogombewa katika Seneti za Vyuo na Vyuo Vikuu ngazi ya mkoa ni pamoja na:
- Mwenyekiti wa Seneti Mkoa
- Katibu wa Seneti Mkoa
- Katibu Hamasa wa Seneti Mkoa
- Wajumbe wawili wa Kamati ya Uratibu ya Seneti Mkoa
Aidha, kutachaguliwa wajumbe watatu (3) kutoka kila wilaya wanaotoka katika matawi ya vyuo na vyuo vikuu, ambao watawakilisha katika Baraza la UVCCM katika wilaya husika kote Tanzania Bara na Zanzibar.
Sifa za Waombaji
Akizungumza kuhusu sifa za waombaji, Mabula amebainisha kuwa mgombea anatakiwa:
- Awe mwanachama wa CCM na UVCCM
- Awe mwanafunzi wa chuo cha kati au chuo kikuu
- Awe amebakiza angalau miaka miwili ya masomo
Sifa nyingine zimeainishwa katika Kanuni ya UVCCM ya mwaka 1978, toleo la 2025.
Wito kwa Vijana
Mabula ametoa wito kwa vijana wote wanaokidhi vigezo hivyo kutumia fursa hiyo kujenga uwezo wao wa kiuongozi na kushiriki kikamilifu katika harakati za jumuiya, akisisitiza kuwa UVCCM ni jukwaa muhimu la kukuza na kuandaa viongozi wa baadaye wa chama na taifa.
Ziara ya Mafunzo UDOM
Kauli hiyo ilitolewa wakati wa ziara ya mafunzo ya Tawi la CHSS, IDS na CI–UDOM, ambalo lilitembelea Makao Makuu ya UVCCM likiwa na wanachama wapya zaidi ya 100.
Katika ziara hiyo, wanachama hao walipata fursa ya kujifunza historia ya Jumuiya ya Umoja wa Vijana wa CCM na Chama Cha Mapinduzi, pamoja na kukabidhiwa kadi za uanachama.
Ziara hiyo imetajwa kuwa ni sehemu ya mkakati wa UVCCM wa kuimarisha uelewa wa misingi ya chama, kuongeza uanachama, na kuhamasisha ushiriki mpana wa vijana wa vyuo katika uongozi na ujenzi wa chama.
Habari Zinazohusiana
UVCCM WILAYA YA KAKONKO WAFANYA MAADHIMISHO YA MIAKA 49 YA KUZALIWA KWA CCM
01 Feb, 2026
Umoja wa Vijana wa Chama Cha Mapinduzi (UVCCM) Wilaya ya Kakonko umefanya maadhimisho ya kipekee kuelekea miaka 49 ya kuzaliwa kwa CCM, yatakayofanyika rasmi tarehe 5 Februari 2026. Maadhimisho haya yamejumuisha shughuli mbalimbali za kijamii zenye lengo la kuunga mkono maendeleo ya wananchi na taifa kwa ujumla.
UVCCM Mufindi yaadhimisha Miaka 49 ya CCM kwa Baraza maalum, yasifu Mchango wa Vijana katika kutafuta ushindi kwa CCM
31 Jan, 2026
Katika kuelekea maadhimisho ya miaka 49 ya kuzaliwa kwa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Umoja wa Vijana wa CCM (UVCCM) Wilaya ya Mufindi umeanza maadhimisho hayo kwa kufanya baraza maalum lenye lengo la kuwapongeza na kuwashukuru vijana wa chama kwa mchango wao mkubwa katika kazi ya kutafuta kura wakati wa Uchaguzi Mkuu uliofanyika Oktoba mwaka jana.
UVCCM Ngome waadhimisha Kuzaliwa CCM kwa Vitendo, wasafisha Soko la Ngome Iringa
31 Jan, 2026
Vijana wa Umoja wa Vijana wa Chama Cha Mapinduzi (UVCCM) Tawi la Ngome, Kata ya Kihesa, Wilaya ya Iringa Mjini mkoani Iringa, wamefanya shughuli ya usafi wa mazingira katika Soko la Ngome kama sehemu ya maandalizi ya maadhimisho ya siku ya kuzaliwa ya Chama Cha Mapinduzi (CCM).